Waziri Wa Ulinzi Marekani Atoa Tamko Zito Kuhusu Irani, Atoa Onyo kwa Vyombo vya Habari – Video
2026-03-02 - 16:58
Waziri wa Ulinzi wa Marekani, Pete Hegseth. Waziri wa Ulinzi wa Marekani, Pete Hegseth, amesema dhamira kuu ya mashambulizi ya Marekani dhidi ya Iran ni kuharibu miundombinu ya kijeshi na kuhakikisha taifa hilo halizalishi silaha za nyuklia. Akitoa taarifa kwa umma leo Machi 2 kuhusu operesheni ya kijeshi iliyopewa jina la Operation Epic Theory, Hegseth alisema operesheni hiyo inalenga moja kwa moja uwezo wa kijeshi wa Iran. “Dhamira ya misheni ‘Epic Theory’ ni mahsusi kabisa — kuharibu miundombinu ya kushambulia ya Iran, kuharibu miundombinu ya kuzalisha silaha, kuharibu jeshi lao la wanamaji na miundombinu mingine ya kiusalama. Iran haitawahi kuwa na silaha za nyuklia,” alisema. Hegseth alieleza kuwa kadri siku zinavyosonga mbele, uwezo wa kijeshi wa Marekani unaimarika zaidi huku ule wa Iran ukizidi kudhoofika kutokana na mashambulizi yanayoendelea. Katika kauli iliyotafsiriwa kama hamasa kwa wananchi wa Iran, waziri huyo alisisitiza kuwa “wakati wao ni sasa kuchukua hatua,” akimaanisha mabadiliko ya ndani dhidi ya uongozi wa sasa. Aidha, Hegseth alivitahadharisha vyombo vya habari dhidi ya kuripoti kuwa vita hivyo vinaelekea kudumu kwa muda mrefu, akivitaka “kuacha mara moja” kusambaza taswira hiyo. Kauli hizo zinakuja wakati mvutano kati ya Marekani na Iran ukiendelea kuongezeka, huku pande zote zikionyesha msimamo mkali kuhusu usalama wa kikanda na suala la silaha za nyuklia.