TheTanzaniaTime

Watoto Wawili Wauawa Serengeti, Mtuhumiwa Auwawa na Wananchi

2026-02-12 - 09:59

Wakazi wa Kijiji cha Rung’abure, Wilaya ya Serengeti mkoani Mara, wamekumbwa na tukio la kusikitisha la mauaji ya watoto wawili yaliyotokea Februari 10, 2026 majira ya saa 11 alfajiri katika Kitongoji cha Getasamo. Watoto hao wametambulika kwa majina ya Mwikwabe Saina (10), mwanafunzi wa darasa la tatu, na mdogo wake Joseph Saina (4). Inadaiwa kuwa walishambuliwa kwa kitu chenye ncha kali na kijana aitwaye Joseph Marwa (18), mkazi wa kijiji hicho. Kwa mujibu wa taarifa za awali kutoka kwa vyombo vya dola, chanzo cha tukio hilo kinahusishwa na imani potofu za kishirikina. Inasemekana mtuhumiwa alimtuhumu mama wa watoto hao kujihusisha na vitendo vya kishirikina dhidi ya ndugu zake, jambo lililoelezwa kuwa lilichochea tukio hilo. Baada ya tukio, baadhi ya wananchi walifanikiwa kumkamata mtuhumiwa na kuanza kumshambulia kabla ya Jeshi la Polisi kufika eneo la tukio na kumuokoa. Hata hivyo, kutokana na majeraha aliyoyapata, mtuhumiwa alikimbizwa katika Hospitali ya Rufaa ya Wilaya ya Nyerere (DDH) Mugumu kwa matibabu, ambako baadaye alifariki dunia. Jeshi la Polisi Mkoa wa Mara limethibitisha kutokea kwa tukio hilo na kueleza kuwa uchunguzi unaendelea ili kubaini mazingira kamili ya tukio hilo pamoja na hatua za kisheria zitakazochukuliwa kwa wote watakaobainika kuhusika, ikiwemo waliohusika katika kitendo cha kujichukulia sheria mkononi. Tukio hilo limezua huzuni na taharuki miongoni mwa wakazi wa eneo hilo, huku viongozi wa jamii wakitoa wito wa amani na kuwataka wananchi kuachana na imani potofu pamoja na vitendo vya kujichukulia sheria mkononi.

Share this post: