TheTanzaniaTime

Watanzania Wawili Watuhumiwa Kujihusisha na Ugaidi Kenya

2026-02-07 - 18:09

Mamlaka nchini Kenya zimetangaza kuwa Watanzania wawili ni miongoni mwa watu 13 wanaotuhumiwa kujihusisha na makosa ya kufadhili ugaidi katika ukanda wa Afrika Mashariki, na kwamba wanakabiliwa na mashtaka pamoja na vikwazo vya kiuchumi. Kwa mujibu wa ripoti iliyotolewa kwa vyombo vya habari nchini Kenya, mamlaka zimesema watuhumiwa hao 13 — wakiwemo Wakenya 10, Mganda mmoja na Watanzania wawili — wanachunguzwa kwa tuhuma za kuhusika na shughuli za kigaidi, ikiwemo ufadhili wake. Majina yao yamewasilishwa kwa taasisi mbalimbali zikiwemo benki na vyombo vya usalama kwa ajili ya kuchunguza kwa kina vyanzo vya fedha walizonazo pamoja na matumizi ya fedha hizo. Hatua hiyo itazilazimu benki husika kusimamisha akaunti za watuhumiwa hao na kutoa taarifa muhimu kuhusu akaunti hizo kwa vyombo vya usalama nchini Kenya. Aidha, taasisi za kifedha ikiwemo mashirika ya mikopo na watoa huduma nyingine za kifedha zimeelekezwa kutojihusisha na shughuli zozote za kibiashara na watu hao hadi uchunguzi utakapokamilika. Kamati maalum ya Baraza la Mawaziri inayoshughulikia masuala ya ugaidi na ufadhili wake nchini Kenya imesema kuwa akaunti za benki za watuhumiwa hao zinapaswa kufungiwa mara moja. Serikali ya Kenya, kupitia Kituo cha Kuripoti Uhalifu wa Kifedha (Financial Reporting Centre), tayari imeorodhesha majina ya watu wote 13 wanaohusishwa na tuhuma hizo. Watanzania waliotajwa katika orodha hiyo ni Salehe Burhani Minja na Jerumani Koja. Kutoka Kenya ni Violet Kemunto Omwoyo, Juma Ambare, Zakariya Kamal, Sufi Abasheikah, Jamal Abdi Mohammed, Hadija Issack Ali, Abdiweli Dubat Dege, Ramadhani Hamisi Kufungwa, Robert Karani Nyokae, Suena Nakhumicha Machabe na Mohammed Siyat Ali, huku raia pekee wa Uganda aliyerodheshwa ni Abubakar Swaleh.

Share this post: