Video: Ndugu Wa Familia Moja Washikiliwa Kwa Tuhuma Za Mauaji Mbeya
2026-02-10 - 13:39
Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya linawashikilia ndugu wa familia moja wakazi wa Busoka–Masebe kwa tuhuma za kumuua Jenti Segelela (87), mkazi wa eneo hilo. Watuhumiwa hao ni Solomon Mwambyale (68) pamoja na watoto wake wawili, Stephano Mwaisango (32) na Emmanuel Mwaisango (36). Kwa mujibu wa taarifa ya Polisi, tukio hilo lilitokea Februari 7, 2026 katika Kitongoji cha Busoka, Kijiji cha Lusungo, Kata ya Makwale. Inadaiwa kuwa watuhumiwa walihusika katika tukio hilo na baada ya kutekeleza tukio walitoroka eneo la tukio. Baada ya tukio hilo, Jeshi la Polisi kupitia askari wake wa upelelezi lilianza msako mkali na kufanikiwa kuwakamata watuhumiwa wote watatu Februari 8, 2026 majira ya saa 7 usiku. Uchunguzi wa awali umebaini kuwa chanzo cha tukio hilo kinahusishwa na mgogoro wa mashamba ya ukoo pamoja na tamaa ya kujipatia mali kwa njia isiyo halali. Uchunguzi zaidi unaendelea ili kubaini ukweli wa tukio hilo kabla ya hatua za kisheria kuchukuliwa. Jeshi la Polisi Mkoa wa Mbeya limeendelea kutoa wito kwa wananchi kutatua migogoro yao kwa njia za amani na kisheria, pamoja na kutoa taarifa kwa vyombo vya dola pindi wanapobaini viashiria vya uhalifu.