TheTanzaniaTime

Uber Yatangaza Kuondoka Nchini, Huduma Yasitishwa Januari 30, 2026

2026-02-01 - 11:29

Kampuni ya kimataifa ya usafirishaji, Uber, imetangaza rasmi kusitisha huduma zake nchini kuanzia Januari 30, 2026, siku ambayo tangazo hilo limetolewa. Kwa mujibu wa taarifa rasmi iliyotolewa na kampuni hiyo, Uber imeeleza kuwa uamuzi huo umetokana na tathmini ya kina ya mazingira ya biashara, huku ikisisitiza kuwa haukuwa uamuzi rahisi kufikia. Kampuni hiyo imetoa shukrani za dhati kwa wateja wake wote, madereva washirika pamoja na wadau mbalimbali waliounga mkono huduma zake tangu ilipoanza kufanya kazi nchini. “Tunawashukuru wateja wetu kwa kutuamini na kutumia huduma zetu kwa kipindi chote tulichokuwepo. Tunaomba radhi kwa usumbufu wowote ambao unaweza kujitokeza kutokana na kusitishwa kwa huduma hizi,” ilieleza sehemu ya taarifa hiyo. Hatua ya Uber kusitisha huduma zake imeibua maswali miongoni mwa watumiaji na madereva wake nchini, hasa ikizingatiwa mchango wake katika sekta ya usafiri wa kidijitali na ajira kwa vijana. Hata hivyo, kampuni haikutoa maelezo ya kina kuhusu iwapo kuna uwezekano wa kurejea tena sokoni hapo baadaye. Kusitishwa kwa huduma za Uber kunatarajiwa kuacha pengo katika soko la usafiri wa mtandaoni, huku wadau wakisubiri kuona namna kampuni nyingine zitakavyotumia fursa hiyo.

Share this post: