TheTanzaniaTime

Ruwa’ichi Atangaza Ratiba ya Mazishi ya Kardinali Pengo, Waumini Waombwa Kujitokeza Kumuaga

2026-02-23 - 14:08

Askofu Mkuu wa Jimbo Kuu Katoliki la Dar es Salaam, Mhashamu Jude Thaddaeus Ruwa’ichi, ametangaza kuwa heshima za mwisho kwa mwili wa Hayati Mwadhama Polycarp Kardinali Pengo zitatolewa siku ya Ijumaa, Februari 27, 2026 katika Kanisa Kuu la Mtakatifu Joseph. Akizungumza na waandishi wa habari leo Februari 23, 2026, Askofu Ruwa’ichi amesema kuwa ratiba hiyo itaambatana na misa maalum zitakazofanyika kanisani hapo pamoja na mkesha wa kumuombea marehemu Kardinali Pengo. Ameeleza kuwa Kanisa Katoliki limesikitishwa sana na kifo hicho, akibainisha kuwa Kardinali Pengo amekuwa mtumishi mwaminifu katika Jimbo Kuu la Dar es Salaam tangu mwaka 1990, akitoa mchango mkubwa wa kiroho na kijamii kwa waumini na taifa kwa ujumla. Aidha, Askofu Ruwa’ichi amefafanua kuwa Kardinali Pengo alikuwa akisumbuliwa na maradhi kwa muda mrefu, ikiwemo matatizo ya moyo na uti wa mgongo. Kwa mujibu wa taarifa hiyo, Kardinali Pengo anatarajiwa kuzikwa siku ya Jumamosi, Februari 28, 2026, katika makaburi ya Pugu, eneo ambalo alikwishajijengea kaburi lake miaka kadhaa iliyopita. Kanisa limewaomba waumini na Watanzania kwa ujumla kuendelea kumuombea marehemu na kuiombea familia pamoja na Kanisa katika kipindi hiki cha maombolezo.

Share this post: