Obama na Clinton Wataka Wamarekani Kusimama Kutetea Maadili ya Taifa
2026-01-28 - 03:05
Marais wa zamani wa Marekani, Barack Obama na Bill Clinton, wamewahimiza Wamarekani kusimama na kutetea kile walichokiita “maadili ya msingi ya Marekani” baada mawakala wa uhamiaji wa Shirikisho huko Minneapolis kumpiga risasi na kumuua muuguzi wa chumba cha wagonjwa mahututi (ICU), Alex Pretti. Mwanamume huyo aliyekuwa na umri wa miaka 37 alipigwa risasi na kuuawa Jumamosi wakati maafisa wa Shirikisho walipokuwa wakijaribu kumkamata. Tukio hilo ni la pili la kuuawa raia wa Marekani na maafisa wa uhamiaji huko Minneapolis mwezi huu pekee, baada ya Renee Good, mama wa watoto watatu, ambaye pia alikuwa na umri wa miaka 37, kuuawa ndani ya gari lake mapema Januari. Katika taarifa yao ya jana Jumatatu, Barack na Michelle Obama walitataja mauaji ya Pretti kuwa ni “msiba wa kuhuzunisha” na kusema yanapaswa kuwa “wito wa kumzindua kila Mmarekani, bila kujali chama chake, kwamba maadili yetu mengi ya msingi kama taifa yanazidi kushambuliwa.” Wamekosoa mbinu zisizo za kawaida za Idara ya Usalama wa Nchi, wakisema kwamba “watu kote nchini wameghadhabishwa kwa haki na tukio la mawakala wa Uhamiaji na Utekelezaji wa Forodha (ICE) waliovaa barakoa na maajenti wengine wa Shirikisho wanaofanya makosa bila kuadhibiwa na kushiriki katika mbinu zinazoonekana kuwa zimebuniwa kuwatisha, kuwanyanyasa, kuwachokoza na kuhatarisha maisha ya wakazi wa mji huo mkubwa wa Marekani. Saa chache baadaye, Bill Clinton pia alitoa maoni yake, akiyataja matukio ya Minneapolis kuwa ya kutisha. Clinton alisema kwamba wasimamizi wanaudanganya umma na kuwaambia “wasiamini kile walichokiona kwa macho yao wenyewe,” akiongeza, “Ni juu yetu sote tunaoamini katika ahadi ya demokrasia ya Marekani kusimama, kuzungumza na kuonyesha kwamba taifa letu bado ni letu Wananchi.” Bill Clinton amesema, “Yote haya hayakubaliki,” huku akiwahimiza Wamarekani “kusimama na kutoa neno.” Umati wa watu ulikusanyika jana Minneapolis, Marekani kupinga uwepo wa maafisa wa uhamiaji wa Shirikisho katika jimbo hilo, baada ya kupigwa risasi na kuuawa Alex Pretti.