TheTanzaniaTime

Museveni – ”Nchi Kubwa Zinaweza Kutaka Kutushinikiza, Tusirudie Makosa”

2026-02-07 - 13:50

Rais wa Uganda, Yoweri Kaguta Museveni, leo Februari 07, 2026 amewasili nchini Tanzania kwa ziara ya siku moja, ikiwa ni ziara yake ya kwanza tangu kufanyika kwa uchaguzi mkuu nchini Uganda. Rais Museveni amepokelewa na mwenyeji wake, Rais wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania, Samia Suluhu Hassan, katika Viwanja vya Ikulu jijini Dar es Salaam. Ziara hiyo imejikita katika majadiliano ya masuala mbalimbali yenye maslahi ya pande zote mbili, yakiwemo uwekezaji katika mradi mkubwa wa bomba la mafuta pamoja na masuala ya usalama wa kikanda. Kupitia ziara hiyo, Rais Museveni alipata fursa ya kuhutubia na kueleza historia ya urafiki wa muda mrefu kati ya Uganda na Tanzania, pamoja na msimamo wake wa kuamini maendeleo ya pamoja ya bara la Afrika. Aidha, Rais Museveni alibainisha kuwa mataifa makubwa yanaweza kuwa na nia ya kuingilia mambo ya ndani ya bara la Afrika, lakini alisisitiza umuhimu wa nchi za Afrika kusimama imara, kushikilia misimamo yao na kuepuka kulegea. Katika kuelezea hilo, alitolea mfano wa nchi ya India ambayo ilikataa kuingiliwa na mataifa makubwa, hatua iliyochangia kuifanya kuwa miongoni mwa mataifa makubwa yenye nguvu na ushawishi mkubwa duniani hadi leo.

Share this post: