TheTanzaniaTime

Mahakama Kuu Yafuta Matumizi ya Mashahidi wa Kificho Katika Kesi za Jinai

2026-02-17 - 10:29

Mahakama kuu ya Tanzania, Masjala Ndogo ya Mwanza, imefutilia mbali utaratibu wa kutumia mashahidi wa kificho katika kesi za jinai nchini kwa kuwa utaratibu huo ni kinyume cha katiba ya nchi. Uamuzi huo umetolewa jana na jopo la majaji watatu ambao ni Jaji Fahamu Mtulya, Jaji Stanley Kamana na Jaji Wilbert Chuma. Mahakama imefuta Kifungu cha 194 cha sheria ya mwenendo wa makosa ya jinai (CPA) ambacho kilimruhusu Mkurugenzi wa mashitaka (DPP) kuomba ulinzi wa mashahidi wa kificho au wa siri. Mahakama imesema utaratibu huo unamlinda Shahidi lakini unamyima haki mshtakiwa na hivyo unaondoa usawa katika kesi za jinai. Awali upande wa waleta maombi ulisema utaratibu wa kutumia mashahidi wa kificho unarahisisha udanganyifu, kwa kuwa mtu mmoja anaweza kutoa ushahidi mara nyingi kwa kutumia majina tofauti, na akalindwa kwa sababu haonekani, jambo ambalo linakiuka haki za msingi za mshtakiwa. Mahakama imetoa muda wa miezi 12 kwa ofisi ya mwanasheria mkuu wa serikali (AG) kufanya marekebisho yanayohitajika kwa kuondoa kifungu hicho cha sheria kinachokiuka katiba ili pasiwepo na shahidi wa siri/kificho mahakamani. Kesi hii ya kikatiba namba 22482/2025 ilifunguliwa na kundi la mawakili 13, likiongozwa na Wakili Mwandamizi Constantine Mutalemwa kwa niaba ya mleta maombi, Wakili Godfrey Mjuni Martin Basasingohe, dhidi ya Mwanasheria mkuu wa serikali (AG) na Mwendesha mashtaka mkuu wa serikali (DPP).! Stori na Elvan Stambuli, Global Digital

Share this post: