TheTanzaniaTime

ACT-Wazalendo Wapinga Maelezo ya Polisi Kuhusu Kifo cha Diwani Buhigwe

2026-01-27 - 10:57

Utata umeibuka kufuatia kifo cha Diwani wa Kata ya Nyamugali, Halmashauri ya Wilaya ya Buhigwe, Majaliwa Abbas Hamis, baada ya chama chake cha ACT-Wazalendo kutilia shaka chanzo cha kifo hicho huku Jeshi la Polisi likisema kimetokana na ajali ya pikipiki. Kupitia ukurasa wake rasmi wa Instagram, ACT-Wazalendo wamedai kuwa mazingira ya kifo hicho yanatia shaka, wakieleza kuwa mwili wa marehemu haukuwa na majeraha yanayoashiria ajali, koti lake lilikutwa pembeni ya mwili, simu yake haikuwa na laini na shingoni kulionekana alama zinazofanana na kunyongwa. Chama hicho kimetaka kufanyika kwa uchunguzi huru na wa kina ili kubaini ukweli. Kwa upande wao, Polisi Mkoa wa Kigoma wamesema uchunguzi wao unaonesha kuwa kifo hicho kilitokana na ajali ya barabarani iliyotokea Januari 23, 2026 majira ya saa nne usiku katika Kijiji cha Songambele. Polisi wamedai marehemu alikuwa akiendesha pikipiki aina ya Kinglion namba MC 709 BCW akiwa amebeba mahindi, ambapo aligongwa na gari lisilofahamika na kufariki dunia papo hapo. Jeshi la Polisi limesema taratibu zote za kiuchunguzi zilifanyika eneo la tukio na vielelezo vilikusanywa, huku simu ya marehemu ikisaidia kutambua utambulisho wake. Polisi wameendelea kusisitiza kuwa kifo hicho ni ajali, kinyume na madai ya ACT-Wazalendo. MBWAMBO AJIUA KWA KUJIKATA KOROMEO AKIWA AMELEWA ‘GUEST HOUSE’ – KAMANDA MORO WAFUNGUKA...

Share this post: